JAFO AHIMIZA SEKTA YA VIWANDA KUUNGWA MKONO KUFANIKISHA JITIHADA ZA RAIS KATIKA UWEKEZAJI WA VIWANDA NCHINI

0

Na Alex Sonna, DODOMA

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dkt. Selemani Jafo ameonesha kutofurahishwa na kiwango kidogo cha watanzania kutumia mbolea ya Kiwanda ya cha Intracom kilichopo Nala jijini Dodoma ambacho kimetokana na matunda ya ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan alipokuwa nchini Burundi.

Akizungumza leo Julai 8, 2024 alipofanya ziara kwenye kiwanda hicho, Waziri Jafo amesema kina uwezo wa kuzalisha tani milioni Moja kwa Mwaka na mahitaji ya Mbolea kwa mujibu wa wizara ya kilimo ni tani 700,000 na kwamba kiwango kilichozalishwa kwasasa takwimu kinaonesha kiwango kidogo kimeuzwa nchini.

“Kwenye taarifa nimeona kuna uzalishaji uliofanyika wa tani 76000 na kati ya hizo tani 60,000 ziliuzwa na zilizouzwa hapa nchini pekee ni tani 4000, sijafurahishwa na hali hii kama Rais amehangaika hadi kuleta kiwanda hiki nchini Mimi nikiwa Waziri wa Viwanda sitakubali hata kidogo juhudi zake zipotee,”amesema.

Dkt. Jafo ameongeza kwa “Sijafurahishwa na mwenendo huu, tunafanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya kilimo Rais ameongeza bajeti ya kilimo kutoka Sh.Bilioni 294 hadi Sh.Trilioni 1.2 ni wazi Rais ana matamanio makubwa sana, niwaombe watanzania kutumia mbolea ya kiwanda hichi,”amesema.

Amebainisha kuwa kiwanda hicho kwasasa tayari uwekezaji wake ni zaidi ya Sh.Bilioni 500 na ujenzi bado unaendelea maeneo mengine na inatarajiwa uwekezaji uwe zaidi ya Sh.Trilioni moja.

Amesema matumizi ya Mbolea nchini yanapaswa kuendana na uzalishaji uliopo kwasasa.

“Kiwanda kwasasa kina waajiriwa 907 na zaidi ya 600 ni watanzania, na kitakapokamilika uwezo wake ni kuajiri watu 3000 Hadi 4000, haiwezekani mbolea izalishwe hapa isinunuliwe Tanzania hii ni kumkwamisha Rais, kwanini tununue mbolea maeneo mengine nje ya nchi lakini tushindwe kununua hapa nchini.”

“Mimi Waziri wa Viwanda sitakubali hata kidogo kuona viwanda vinavyojengwa Tanzania vinashindwa kuwezeshwa kufanya kazi yake hii kubwa, sisi kama serikali tutajadiliana namna ya kufanya ili viwanda vinavyojengwa nchini vifanye kazi vizuri,”amesema.

Amewahakikishia wawekezaji kuwa atasimamia kuhakikisha viwanda vilivyowekezwa nchini vinakidhi matarajio ya Rais.

“Tutavilinda viwanda vyetu hapa nchini vifanye kazi vizuri na vijana wetu wapate ajira na dhamira ya Rais Samia ya kuhangaika kutafuta wawekezaji lazima itimie,”amesema.

Naye, Mkurugenzi wa Kiufundi wa Kiwanda hicho, Mhandisi Victor Ngendazi, amesema kiwanda hicho kilianza kujengwa Julai 2021 na lengo lilikuwa kutengeneza mbolea tani 600,000 lakini kutokana na maombi ya serikali ya Tanzania wameongeza hadi tani milioni moja.

“Kwasasa ujenzi unaendelea kwenye maeneo yaliyosalia tunataka eneo hili tuwe na viwanda vitano na tayari vitatu vinafanya kazi na uzalishaji kwa ujumla utaanza mwezi Agosti Mwaka huu baada ya kukamilisha majaribio ya mitambo ya viwanda viwili,”amesema.

Amesema wamekuwa wakishirikiana na serikali kutatua changamoto zilizokuwapo zikiwakabili na kusisitiza uwezo wa uzalishaji upo wa kutosha.

“Changamoto tunayopata ni wakati wa mauzo, Tanzania kwenye tani zilizozalishwa tumeuza tani 4000 wakati Kenya wamenunua tani 52,000 na Burundi tani 10,000 unaweza kuona kwa Tanzania tupo nyuma sana, tunaomba katika mikakati ya Serikali ya kulinda viwanda vya ndani ruzuku isiende sana kwenye mbolea za kutoka nje ije kwenye viwanda vilivyowekezwa hapa nchini,”amesema.

Amesema uwezo wa Kiwanda ni mkubwa na kama wataendelea kukosa soko watasimamisha uzalishaji.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *