NAIBU WAZIRI SANGU AITAKA MAMLAKA YA SERIKALI MTANDAO KUWAUZA VIJANA WABUNIFU WA TEHAMA

0

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu ameitaka Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kushiriki kwenye Maonesha mbalimbali ya Ubunifu ili kuonesha uzuri wa mifumo iliyobuniwa pamoja na umahiri wa vijana walioandaliwa na Taasisi hiyo ili vijana hao waweze kupata soko kwenye Sekta Binafsi.

Ametoa kauli hiyo leo wakati akifunga mafunzo kwa vitendo kwa Wanafunzi 65 wa Vyuo Vikuu mbalimbali yaliyofanyika kwa kipindi cha muda wa wiki kumi katika Kituo cha Ubunifu na Utafiti cha eGA kilichopo jijini Dodoma.

Ameitaka eGA kutekeleza program hiyo ya kukuza ubunifu katika TEHAMA kwa wanafunzi wa Elimu ya juu kimkakati kwa kuwakutanisha vijana hao na Waajiri ambao ni sekta binafsi.

Kufuatia hatua hiyo Mhe.Sangu ameitaka eGA kuimarisha ushirikiano zaidi na Sekta binafsi ili vijana wanaoandaliwa na Taasisi hiyo waweze kukidhi hitaji la soko la ndani na nje ya nchi katika eneo la Tehama bunifu.

” Nimefarijika kusikia Benki ya NMB pamoja na Kampuni ya Vodacom ni miongoni mwa washirika wenu ambao mnashirikiana nao kwa kuwaeleza mahitaji ya soko na hivyo kuisaidia jinsi ya kuwapika vijana ili waendane na hitaji la soko” amesema Mhe.Sangu

Ameongeza kuwa ” Nimeambiwa mwaka jana Benki ya NMB ilichukua jumla ya vijana nane mliowaandaa, hii ni habari njema sana kwetu kama Serikali”

Katika hatua nyingine, Mhe.Sangu ameitaka eGA kuandaa kanzidata kwa vijana wote wanaopata mafunzo kwa vitendo katika Kituo hicho badala ya kuwaacha tu bila ya kuwa na taarifa zao.

Amesema ili kuhakikisha TEHAMA inatoa matokeo tarajiwa kwa Uchumi wa nchi ya Tanzania vijana hao wanadiwe kwa bunifu zao wanazofanya Ili kuweza kuwashawishi waajiri.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Eng. Benedict Ndomba amesema kuwa Kituo hicho kimekuwa kikifanya tafiti katika maeneo yote ya TEHAMA kwani tafiti hizo na bunifu zinaiweka nchi katika nafasi nzuri ya kushindana kwenye Uchumi wa kidijitali na Mataifa mengine.

Naye, Jane Claud ambaye ni mwanafunzi aliyepata mafunzo kwa vitendo katika Kituo hicho licha ya kushukuru kwa kupata fursa hiyo ameiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa kituo kikubwa ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia yanatokea duniani

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *