WAENDELEZAJI MIRADI YA NISHATI JADIDIFU WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA KUTOKA REA

0
IMG-20250619-WA0012

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu ametoa wito kwa waendelezaji wa miradi ya nishati jadidifu kote nchini kuchangamkia fursa za uwezeshwaji zinazotolewa na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ili kuwa na miradi yenye tija kwa Taifa.

Ametoa wito huo Juni 19, 2025 akiwa kwenye ziara ya kutembelea na kukagua mradi wa kuzalisha umeme wa Mwenga wa megawati nne unaomilikiwa na Kampuni ya Mwenga Hydro Limited kwa kutumia maporomoko ya Mto Mwenga katika Kijiji cha Ifwagi, Wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa.

“Kwenye eneo hili la nishati jadidifu fursa zilizopo ni nyingi, Tanzania ni kubwa na imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi na bado hazijatumika ipasavyo; tunahitaji waendelezaji wengi wa miradi ya kuzalisha umeme kwa upepo, joto ardhi, jua na maporomoko ya maji kujitokeza ili kuwezeshwa na REA kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa umeme nchini,” alisema Mhe. Balozi Kingu.

Alisisitiza kuwa waendelezaji wa miradi ya nishati jadidifu ni muhimu katika kuharakisha maendeleo ya Taifa hasa ikizingatiwa kuwa umeme ni miongoni mwa nyenzo muhimu katika kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya Taifa.

Alisema tangu REA imeanza kuwezesha waendelezaji wa miradi hiyo ya nishati jadidifu mchango wao umeonekana kuanzia ngazi ya chini ya eneo la mradi ambao umenufaisha vijiji vinavyozunguka hadi ngazi ya Taifa kupitia umeme wanaoingiza katika Gridi ya Taifa.

“Waendelezaji wadogo wa miradi hii ni muhimu kwani mchango wao kwa Taifa unaonekana; sisi tunaahidi kuendelea kuwaunga mkono kwa kuwawezesha kwa namna mbalimbali ikiwemo ruzuku pamoja na mikopo nafuu ya muda mrefu sambamba na kuwajengea uwezo wa kitaalamu,” alifafanua Mhe. Balozi Kingu.

Akizungumzia mradi huo wa Mwenga, Mhe. Balozi Kingu alisema Bodi anayoiongoza inajivunia mchango wa REA katika mradi na alitoa wito kwa uongozi wa mradi kuwasilisha andiko la kuongeza Kasi ya upatikanaji wa umeme nchini.

“Nimeelezwa mmepata chanzo kingine cha kuzalisha umeme ambacho kinaweza kutupatia takriban megawati 10, fanyeni hima kuwasilisha andiko lake ili nasi tuanze taratibu stahiki; tunahitaji mirdi mingi ya namna hii ili kuliongezea nguvu Shirika la Umeme (TANESCO),” alisema.

Akiwasilisha taarifa ya Mradi, Mkurugenzi wa Kampuni ya Rift Valley Energy kampuni mama ya Mwenga Hydro Limited, Michael Gratwicke aliishukuru REA kwa uwezeshwaji mkubwa iliyofanya katika mradi huo.

“Tunaishukuru REA kwani leo hii tunahudumia takriban kaya 10,000 ndani ya vijiji 32 kutokana na uwezeshwaji wa REA; tusingefika hapa kama isingekuwa uwezeshwaji huu,” alisema Gratwicke.

Akizungumza kuhusiana na uwezeshwaji kwa ujumla, Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage alisema REA ilitoa ruzuku ya takriban shilingi bilioni 23 kuendeleza mradi huo.

“Serikali kupitia REA imewezesha mradi huu kwa kutoa kiasi cha fedha takribani shilingi bilioni 23 ikiwemo shilingi bilioni 18 ya kuwaunganisha wateja na shilingi bilioni 5 ambayo ilitolewa Kama mkopo wa mda mrefu ili kuwezesha ujenzi wa Mradi huo,” alifafanua Mha. Mwijage.

Alisema kuwa Wakala unatoa kipaumbele kwenye ujenzi wa miradi ya nishati jadidifu nchini ili kusaidia utunzaji wa mazingira, kuboresha upatikanaji wa umeme, kuongeza uzalishaji wa umeme unaotokana na nishati Jadidifu pamoja na kutoa ajira kupitia miradi hiyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *