DKT. BITEKO ATAJA MAENEO SITA YA VIPAUMBELE UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM 2020/2025

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita aliyowasilisha ni ya mwisho katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020.
Amesema hayo Mei 29, 2025 wakati akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Mkutano Mkuu Maalum wa CCM Taifa – 2025 jijini Dodoma kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa.
Ametaja maeneo sita muhimu ya vipaumbele katika utekelezaji wa Ilani hiyo ya CCM kuwa ni pamoja na kulinda na kuimarisha misingi ya utu, usawa, haki na uongozi bora ili kudumisha amani, umoja na mshikamano wa Taifa.
Dkt. Biteko ameendelea kwa kusema kuwa eneo lingine ni kukuza uchumi wa kisasa, fungamanishi, jumuishi na shindani uliojengwa katika msingi wa viwanda, huduma za kiuchumi na miundombinu wezeshi.

Aidha, kipaumbele kingine “ Kuleta mageuzi ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kuwa na uhakika wa chakula na kujitegemea kwa chakula wakati wote na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi na kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya, elimu, maji, umeme na makazi vijijini na mijini na kutengeneza ajira zisizopongua milioni nane katika sekta rasmi na isiyo rasmi kwa ajili ya vijana,” ameongeza Dkt. Biteko.
Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesema kuwa kumekuwepo na mafanikio makubwa ikiwemo nchi kuendelea kuwa na amani, umoja na mshikamano pamoja na kuendelea kuenzi Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar na kudumisha Muungano wa Tanzania.
“ Vilevile, Serikali imeendelea kuimarisha demokrasia, utawala bora na haki za binadamu kwa kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuondoa zuio la mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na hivyo kuimarisha uhuru wa vyombo vya habari ili kuwezesha wananchi kupata habari kwa wakati,” amesema Dkt. Biteko.

Ameendelea kusema kuwa mafanikio hayo yamechagizwa na falsafa aliyoianzisha Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya 4R ambayo ni Maridhiano, Ustahimilivu, Mabadiliko na Kujenga Upya.
Amesisitiza “ Falsafa hiyo imekuwa dira na nguzo muhimu ya kisera katika kuijenga upya Tanzania yenye mshikamano, haki na maendeleo endelevu kwa misingi ya demokrasia na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya msingi ya Taifa.”
Kupitia mkutano huo Dkt. Biteko alielezea mafanikio ya Rais Samia kitaifa na kimataifa hususan katika sekta ya nishati kwa kuwa kinara wa nishati safi ya kupikia barani Afrika.
Akihutubia katika mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Mkutano Mkuu huo ni sehemu muhimu ya maandalizi ya kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.
“ Kesho tutafanya uzinduzi wa Ilani tutakayoinadi kwa wananchi ili kutupa nafasi nyingine ya kuongoza kwa miaka mitano,” amesema Dkt. Samia.


Amebainisha kuwa Ilani hiyo imehusisha vipaumbele vya Chama na kuwa kabla ya kuiwasilisha kwa wajumbe wameona ni muhimu kupitia utekelezaji wa Ilani ya mwaka 2020 hadi 2025.
Akizungumza katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa CCM, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema lengo la mkutano huo ni kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa mwaka 2020 hadi 2025, kuzindua Ilani mpya 2025 hadi 2030 na kupitia maboresho machache ya Katiba ya CCM.
Aidha, Mkutano huo ulioongozwa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan umehudhuriwa na viongozi wa vyama vya siasa nchini, mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania pamoja wawakilishi wa vyama rafiki kutoka nchi mbalimbali za Afrika, China na Korea ya Kaskazini na Urusi.