REA YAENDELEA KUTEKELEZA MKAKATI WA TAIFA WA MATUMIZI YA NISHATI SAFI

0

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea na jitihada mbalimbali za uelimishaji, uhamasishaji na usambazaji wa bidhaa za Nishati Safi za Kupikia katika Mikoa yote Tanzania Bara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kwa lengo la  kuhakikisha 80% ya Wananchi wanatumia Nishati Safi za Kupikia ifikapo Mwaka 2034.

Hayo yameelezwa Machi 7, 2025 Jijini Arusha na Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji Miradi REA, Mhandisi Emanuel Yesaya wakati wa Maonesho ya Kuelekea Siku ya Wanawake Duniani 2025.

“Tunashiriki kutoa elimu, kuonyesha bidhaa mbalimbali za nishati safi ya kupikia na kuhamasisha wananchi hususan akina mama kutumia nishati safi ya kupikia ili kurahisisha maisha yao sambamba na kulinda afya zao,” alisema Mhandisi Yesaya

Alisema REA imeandaa program mbalimbali zinazolenga kumrahisishia maisha mwanamke hasa ikizingatiwa kuwa mwanamke ndiye kinara wa jiko.

Alisema Serikali inatambua umuhimu wa kulinda afya za wananchi wake sambamba na kuhifadhi mazingira ambayo kwa kiasi kikubwa yameathiriwa na matumizi ya Nishati chafu za kupikia zikiwemo kuni na mkaa na sasa mwelekeo ni kujikita katika matumizi ya Nishati Safi za Kupikia ambazo Serikali inafanya kila njia zifike kwa kila mwananchi kwa gharama anayoweza kumudu.

“Hii ni fursa adhim ambayo imetolewa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye kinara wa Nishati Safi ya Kupikia kwa wananchi wake, tunatoa rai kwa Watanzania kuchangamkia fursa hii,” alisema Mhandisi Yesaya.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa REA, Bi Martha Chassama alitoa wito kwa wanawake kutembelea banda la Wizara ya Nishati ili kujifunza kwa undani umuhimu wa kutumia Nishati Safi ya Kupikia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *