MHANDISI BWIRE: TUNAIRUDISHA DAWASA KWA WANANCHI

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Mkama Bwire amesema wanakusudia kurejesha Mamlaka hiyo kwa wananchi ili kutoa fursa na na nafasi ya kufikisha mrejesho wa huduma na kutatua changamoto za Maji ili kusaidiwa kwa haraka.
Mhandisi Bwire ameyasema hayo leo Februari 20, 2025 wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi kati ya DAWASA na Wenyeviti wa mitaa wa wilaya ya Temeke na kusema kuwa hiyo ndio agenda ya Mamlaka katika utendaji kazi wao
“Tunekusudia turudishe DAWASA iwe ni ya wananchi tunaamini tukishirikiana pamoja changamoto za kihuduna kupitia Wenyeviti wa mitaa zitaisha” alisisitiza Mhandisi Bwire.


Mhandisi Bwire amesema kupitia kikao hicho watajadili changamoto za maji zilizopo katika maeneo ya Temeke kupokea mawazo na maoni ya wenyeviti juu ya suluhisho lakini kujenga mahusiano yatakayosaidia kuweza kuwa karibu baina ya DAWASA na viongozi hao.
“Lazima tuwe na mambo ambayo tunataka kushirikiana na kujenga uelewa wa pamoja tunapoenda kwa Wananchi kile anachozungumza Mwenyekiti na DAWASA azungumze hivyo” alisisitiza
Aidha Mhandisi Bwire ameongeza kuwa mamlaka hiyo imetambua umuhimu wa wenyeviti na kuelewa nafasi yao katika kurahisisha ufikishaji wa huduma kwa Wananchi na kutatua changamoto zilizopo
Pamoja na hayo Mhandisi Bwire amekiri uwepo wa changamoto mbalimbali katika Manispaa ya Temeke lakini amesema anaamini sasa itakuwa rahisi kutatua changamoto hizo kutokana na uwepo wa uhusiano mzuri baina yao.