DC BAHI AIPONGEZA DUWASA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAJI

0

Mkuu wa Wilaya ya Bahi Rebecca Nsemwa ameipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) kwa kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji wilayani hapo kutoka asilimia 50 kwa mwaka 2021 mpaka kufikia asilimia 100 mwaka 2024.

Ambapo amesema Mafanikio hayo yametokana na Uwekezaji mkubwa uliofanywa na DUWASA tangu mwaka 2020 mpaka 2024 na kuwafanya kutimiza lengo la Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Nsemwa ametoa kauli hiyo leo Septemba 4,2025 wilayani Bahi, wakati akifungua kikao kazi cha Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazngira (DUWASA) na viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Ambapo ametumia wasaa huo kuwasisitiza viongozi wa mitaa kushirikiana na jamii kulinda vyanzo vya maji.

Mkuu wa Wilaya ya huyo amesema Maji hayana mbadala hivyo suala la maji hayana mjadala.

“DUWASA mmefanya kazi nzuri Sana katika Wilaya ya Bahi ila niwaambie ukweli maji hayana mbadala na hayahitaji mjadala ndio maana huwezi kuwaambia wananchi chochote ambao hawana maji zaidi ya kuwapelekea, nawategemea Sana nyinyi kama wataalamu wa sekta ya maji mtusaidie kuwafikishia wananchi huduma ya maji ya uhakika, ” amesema Nsemwa

Pia amewataka DUWASA kuhakikisha wanalipa fidia kwa wale wananchi wanaotoa maeneo yao kwa ajili ya Kupisha miradi ya maji na kuwashirikisha kila hatua inayoendelea katika utekelezaji wa miradi ya maji kwa kutumia viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Pia ameagiza utunzaji wa mazingira ikiwemo vyanzo vya Maji ili kuhakikisha upatikanaji wa maji yanakuwa endelevu.

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa DUWASA Mhandisi Aron Joseph amesema lengo la Mamlaka hiyo ni kuhakikisha huduma ya majisafi inapatikana kwa unakika katika Wilaya ya Bahi huku akiwakikishia viongozi hoa wa Serikali za Mitaa utaratibu wa kupeleka maji ambayo hayana chumvi kupitia mradi wa Ibiwa unaendelea na ukikamilika utaondosha kabisa kero ya maji chumvi wilayani humo.

“Moja ya changamoto tuliyokutana nayo hapa Bahi ni Maji yake kuwa na Chumvi ila kwa sasa utaratibu wa kuleta maji ambayo hayana chumvi kupitia mradi wa Ibiwa unaendelea na ukikamilika utaondosha kabisa kero ya maji chumvi ila ni bora hata maji yakawepo kuliko kutokuwepo kabisa hivyo jitihada kubwa ni kuhakikisha Kwanza maji yanakuwepo Bahi, “ameeleza Mhandisi Aron

Naye Meneja wa DUWASA Kanda ya Bahi Winifrida Massawe amesema mpaka kufikia Agosti 2024 Mamlaka hiyo imewaunganishia maji wateja 568 ambapo wamesambaziwa maji moja kwa moja kutoka kwenye Visima vyao na Matenki yenye uwezo wa kuhifadhi maji Lita laki nne na ishirini na tano ambayo yapo matatu.

DUWASA inafanya mikutano mbalimbali na viongozi wa Serikali za Mitaa katika ngazi ya kijiji mpaka Halmashauri ,wakiwemo wenyeviti na watendaji wa vijiji,kata,madiwani na wakurugenzi wa wilaya kulingana na maeneo ambayo Mamlaka hiyo inahudumia ndani ya Mkoa wa Dodoma.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *