MPANGO AAGIZA FEDHA ZITOLEWE KUKAMILISHA UJENZI WA VETA MPWAPWA

0

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Phillip Mpango amemuagiza Waziri wa Fedha kutoa fedha ili kukamilisha awamu ya kwanza ya ujenzi wa Chuo ya Ufundi Stadi VETA wilaya ya Mpwapwa Mkoani Dodoma ili Chuo hicho kianze kutoa Mafunzo kwa wakati.

Dkt. Mpango ametoa agizo hilo Agosti 20, 2024 alipotembelea eneo kinapojengwa Chuo hicho kukagua maendeleo ya ujenzi ambapo amesema VETA ndio mkombozi wa ajira kwa Vijana.

“Kwa kipaumbele ni muhimu sana tupate Vyuo vya VETA katika Makao Mkuu ya Nchi ambavyo vitaleta athari chanya kwa Vijana wetu na ikawe mfano katika maeneo mengine” Alisema Dkt. Mpango.

Awali akizungumza katika ziara hiyo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda amesema ujenzi wa Chuo hicho ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kujenga Chuo cha VETA cha Serikali katika Wilaya zote nchini ambazo hazikua na vyuo hivyo.

“Kuna Wilaya 64 ambazo ujenzi wa VETA unaendelea pamoja na Chuo kimoja cha hadhi ya Mkoa katika Mkoa wa Songwe ambo ndio mkoa uliokuwa hauna Chuo cha VETA ch Mkoa” alisema Waziri Mkenda.

Awamu ya kwanza ya ujenzi wa VETA Mpwapwa unajumuisha majengo 9 ikiwemo jengo la utawala, madarasa, karakana, nyumba ya Mkuu wa Chuo na jengo la kuweka miundombinu ya umeme.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *