TANZANIA KUWA MWENYEJI WA KONGAMANO LA PILI LA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU UTALII WA VYAKULA VYA ASILI BARANI AFRIKA

0

Tanzania inatarajiwa kuwa Mwenyeji wa Kongamano la Pili la Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii Duniani (UN Tourism), Kanda ya Afrika kuhusu utalii wa vyakula vya asili katika Bara la Afrika kwa mwaka 2025.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii Duniani (UN Tourism), Zurab Pololikashvili katika ufunguzi wa Kongamano la kwanza la Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii Duniani, Kanda ya Afrika kuhusu Utalii wa vyakula vya asili katika Bara la Africa (Gastronomy) linaloendelea jijini Victoria Falls nchini Zimbabwe leo Julai 26, 2024.

Bw.Pololikashvili amemshukuru Waziri wa Maliasili na Utalii wa Tanzania, Mhe. Angellah Kairuki kwa ushirikiano wake na nia yake ya kutaka kutangaza utalii wa chakula na kusisitiza kuwa Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii Duniani liko tayari kutoa ushirikiano kwa nchi za Afrika katika kutangaza utamaduni wa Kiafrika hasa Utalii wa vyakula.

Naye, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) amesema kufanyika kwa Kongamano hilo nchini Tanzania kutakuwa na manufaa makubwa katika kukuza mnyororo mzima wa thamani katika utalii ikiwemo Utalii wa vyakula hasa kugusa wadau wengi wakiwemo wakulima wafugaji, wavuvi,wazalishaji wa nafaka,wachakataji wa mafuta n.k.

“Tunao mwaka mmoja wa kufanya maandalizi na tutajipanga vizuri kuhakikisha kwamba Tanzania inaonesha urithi na utajiri mkubwa tulionao lakini ni nafasi nzuri katika kukuza utalii wetu zaidi” Mhe. Kairuki ameongeza.

Kongamano hilo limefunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, Mhe. Emmerson Mnangagwa ambaye amesisitiza juu ya umuhimu wa Sekta ya Kilimo katika kukuza Utalii wa Chakula.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *