UWANJA MPYA WA NDEGE SHINYANGA KUANZA KUTUMIKA OCTOBA 3, 2024-ENG JOEL

0

Mradi wa Ujenzi wa Uwanja wa ndege wa Shinyanga kwa kiwango cha lami wenye urefu wa kilometa 2.2 ni moja ya mikakati ya Serikali ya awamu ya 6 inayoongozwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika mkoa wa Shinyanga na mikoa jirani, kwa kuboresha mtandao wa safari za anga ili kuongeza ufanisi katika sekta ya usafiri na usafirishaji.

Ujenzi wa uwanja huo utaanza kutumika tarehe 3 Octoba 2024 na pindi utakapokuwa umekamilika utakuwa na uwezo wa kupokea ndege za ukubwa wa Q400.

Ujenzi wa Uwanja wa ndege wa Shinyanga umefadhiliwa kwa ushirikiano wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya, European Investment Bank (EIB) kupitia Wizara ya Ujenzi na Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) inayosimamia utekelezaji wake.

Mkataba wa ujenzi wa uwanja huo ulisainiwa tarehe 30 Juni 2017 na mkandarasi kuanza kazi tarehe 04 Aprili 2023 ambapo muda wa Utekelezaji wa Mradi huo ni Miezi 18 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 49.2

Hayo yamebainishwa na Meneja wa Wakala ya Barabara Tanzania – TANROADS Mhandisi Joel Samwel Mwambungu mara baada ya kutembelea na kukagua hatua zilizofikiwa za ujenzi wa mradi huo.

Mhandisi Joel amezitaja kazi zitakazohusika na mradi huo kuwa ni pamoja na Ujenzi wa njia ya kurukia ndege yenye urefu wa mita 2200 na upana wa mita 30 (Runway), njia ya kuingilia na kutokea ndege (Taxiway) na maegesho ya ndege (Apron) zote kwa kiwango cha lami.

Amezitaja kazi zingine kuwa ni pamoja na Ujenzi wa jengo la abiria (Termina Building) likijumuisha mnara wa kuongozea ndege (Control Tower), Uwekeaji wa taa zq kuongozea ndege (Installation of AG land DME/VOR), Ujenzi wa mitambo ya maji (Storm Water Drainage Systeam), uzio kuzunguka kiwanja, barabara ya mzunguko ndani ya uwanja, na barabara ya kufikia uwanja wa ndege (Access Road).

Mhandisi Joel amesema kuwa mara baada ya mradi huo kukamilika utakuwa kiunganishi muhimu kwa maeneo ya ukanda wa ziwa hasa wananchi wa Shinyanga na maeneo ya jirani waliokuwa wanakosa huduma za usafiri wa anga kwa muda mrefu, na kuvutia wawekezaji na watalii katika mikoa yote ya jirani.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *