WABUNGE WATAKA BAJETI YA UJENZI IPITE, WALILIA IONGEZWE FEDHA

0

Wabunge wamepongeza kazi zinazofanyika katika Wizara ya Ujenzi huku wakitaka Kamati ya Bajeti kufanya mapitio upya ya bajeti ili kuongeza fedha kwa Wizara hiyo.

Waziri wa Ujenzi Innocent Bashungwa jana aliwasilisha bajeti ya Wizara hiyo akiomba bunge lipitishe Sh1.7 Trilioni kwa mwaka 2024/25 kiasi ambacho wabunge wanasema hakitafikia malengo kwani mvua zimeharibu miundombinu katika maeneo mengi hivyo alistahili fedha zaidi ya hizo.

Mbunge wa Nyasa Stella Manyanya amesema hakuna kinachoshindikana ndani ya Wizara hiyo isipokuwa wanakwamishwa na ufinyu wa bajeti waliyopewa ukilinganisha na majukumu ya kuifungua.

Manyanya amesema kuna wasiwasi Waziri wa Ujenzi akaitwa ‘Aristoto’ kwa sababu ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi ambayo ni ndogo kwani hakuna mtu anaweza kufanya masuala ya kiufundi kwa kuangalia philosophy.

Mbunge wa Nyamagana Stanslaus Mabula ametaja miradi mikubwa iliyoonyesha matumaini kwa Wananchi ikiwemo kukamilika kwa Daraja la Usagala, meli za Mv Mwanza na Mv Umoja na Kuboresha Miundombinu ya Bandari kuwa kielelezo tosha cha kuwataka wabunge waunge mkono bajeti hiyo ili Serikali ikatekeleze maeneo yaliyobakia.

Mbunge wa Viti Maalum Stella Fiyao amesema utayari wa Waziri na Naibu Waziri katika kipindi ambacho nchi ilikumbwa na changamoto ya mvua kubwa katika maeneo mengi, kunampa tumaini kuwa Wizara hiyo inastahili pongezi.

Kwa upande wake Mbunge Viti Maalum Mary Masanja amesema Waziri Innocent Bashungwa alionyesha uzalendo mkubwa katika kipindi kigumu ambapo ilimlazimu kupanda pikipiki ili kuyafikia maeneo magumu jambo ambalo si kawaida kwa Waziri.

Hata hivyo Masanja ameomba Serikali kuongeza fedha katika Wizara hiyo ili wananchi waweze kunufaika matunda mazuri ya Serikali yao akidai fedha zilizotengwa kwa 2024/25 hazitoshi.

Akizungumzia magumu yaliyotokana na mvua za Eli-nino, Mbunge wa Liwale Zuberi Kuchauka amesema kazi iliyofanywa na Waziri Bushungwa kwa kutumia chopa na boti ilipeleka matumaini makubwa kwa wananchi wa jimbo lake na mkoa mzima wa Lindi.

Naye Mbunge wa Madaba Dk Joseph Mhagama amempongeza Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wa kutenganisha Wizara ya Uchukuzi na Ujenzi lakini kwa uteuzi wa Waziri mwenye maono anayetambua majukumu yake.

Amesema wananchi wa Madaba na Mkoa wa Ruvuma hawana shaka na utendaji kazi wa Waziri Bashungwa kwakuwa walilijua hilo tangu alipoteuliwa na hivyo akaomba wabunge wapitishe bajeti yake.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *