CHUO KIKUU MZUMBE WAKUTANA NA WADAU WA NJE ILI KUPITIA PROGRAMU YA SHERIA KWA NJIA YA TEHAMA

0

Chuo Kikuu Mzumbe imekutana na wadau wa masuala ya Sheria kutoka Taasisi mbalimbali nchini (External Stakeholders) kwa ajili ya kutengeneza programu ya Sheria ngazi Uzamivu ambayo inatarajiwa kutolewa na chuo hicho kupitia njia ya TEHAMA (Information Computer Technology).

Akizungumza leo Mei 29, 2024 wakati akifungua warsha iliyofanyika katika Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Dar es Salaam, Mkuu wa Idara Masomo ya Biashara Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Dar es Salaam Dkt. Joshua Mwakunjonga, amesema kuwa wabobezi wa sheria kutoka nje ya Chuo hicho (External Stakeholders) wamekuja kupitia programu ya sheria ngazi uzamivu ili waweze kufanya maboresho ambayo yataleta tija katika Taifa.

Dkt. Mwakunjonga amesema kuwa program hiyo inafadhiliwa na Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) ambapo kuna programu nyingi zimetengenezwa kupitia ufadhili huo ambao umelenga kuongeza ufanisi katika nyanja mbalimbali.

“Wamekuja kwa ajili ya kuangalia kama programu ya Master of law with ICT inaendana na uhitaji wa soko, kama kuna kasoro watasema wapi tunapaswa kurekebisha ili iwe bora zaidi na kuleta tija” amesema Dkt. Mwakunjonga.

Dkt. Mwakunjonga amesema kuwa programu hiyo ni mpya ambayo imeonekana ni moja ya mahitaji ya soko, hivyo wanatarajia kuona wanafunzi wengi kuja kusoma kwani ili kuendana na uhitaji wa jamii na kuchangia katika maendeleo ya Taifa.

Chuo Kikuu Mzumbe kupitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni miongoni vya vyuo vikuu nchini ambavyo vimenufaika na Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Uchumi (HEET) ambao umefadhiliwa na Benki ya Dunia.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *