TANESCO KINONDONI KUSINI WATOA ELIMU KWA WANANCHI HUDUMA YA JISOTI

0

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Kinondoni Kusini limeugana na wadau mbalimbali kukimbiza Mwenge wa Uhuru katika Wilaya ya Ubungo pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya njia mpya ya kutoa taarifa kupitia simu janja inayojulikana kwa jina la TANESCO JISOTI ambayo inampa fursa mteja kuwasiliana na mtoa huduma kupitia namba ya WhatApp 0748 550 000.

Akizungumza leo Mei 12, 2024 jijini Dar es Salaam wakati wakitoa elimu ya matumizi ya huduma ya kiganjani ya kuwasiliana na mtoa huduma wa TANESCO katika Viwanja vya Barafu Mburahati, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kinondoni Kusini Mhandisi Florence Mwakasege, amesema kuwa kupitia TANESCO JISOTI mteja ataweza kupata huduma yoyote kutoka TANESCO kupitia simu janja bila kufika katika ofisi zao.

“Lengo la huduma ya TANESCO JISOTI ni kutoa huduma kwa ukaribu na kuhakikisha wateja wetu wanapata huduma bora na kuchochea shughuli za maendeleo” amesema Mhandisi Mwakasege.

Afisa Uhusiano Huduma kwa Waeja TANESCO Mkoa Kinondoni Kusini Samia Chande, amesema kuwa Shirika limejipanga kutoa huduma bora kwa wateja ili kuleta matokeo chanya nakuimarisha hali ya uchumi katika jamii.

Aliongezea kwa kusema kuwa kwa sasa hali ya upatikanaji umeme Nchini imeimarika kutoka na mashine moja yenye uwezo wa kuzalisha takribani Megawatt 235 katika mradi wa Julius Nyerere kuanza uzalishaji.

Nao baadhi ya wakazi wa Wilaya ya Ubungo waliotembelea banda la TANESCO Mkoa wa Kinondoni Kusini wameishukuru Shirika hilo kwa kuleta huduma ya TANESCO JISOTI kwani inakwenda kuwa msaada kwao kwa kuwasiliana na mtoa huduma kwa wakati.
Mkazi wa Wilaya ya Ubungo Eduwin Nyange ameupongeza utendaji wa TANESCO kwani baada ya kufika katika banda lao wamemsikiliza na kumsaidia kutatua changamoto ambayo ilikuwa inamkabili pamoja na kumshauri namna bora ya kuwasiliana na shirika wakati anapoitaji huduma.

Naye Zuhena Marry ambaye alitembelea banda la TANESCO katika viwanja vya Mburahati barafu amesema kuwa amepata faida nyingi baada ya kuonana na wafanyakazi wa TANESCO ikiwemo namna ya kupata huduma mita ya umeme pamoja na namna bora ya kuwasiliana kupitia simu janja JISOTI.

“Nimepata majibu ya maswali yangu kuhusu TANESCO na nimeyafuraia naomba waendelee kutoa elimu kwa jamii ili waweze kuwa na uelewa wa shirika hili ambalo linamchango mkubwa katika kukuza uchumi” amesema Marry

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *