TANESCO TEMEKE WAJENGEWA UWEZO WA MAADILI KUEPUKA VITENDO VYA RUSHWA

0

Watumishi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Temeke wamejengewa uwezo na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Temeke, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa ajili ya kufanya kazi kwa ufanisi ili kuhakikisha wanaepuka vitendo vya rushwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumza leo Aprili 17, 2024 Jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Meneja wa TANESCO Mkoa wa Temeke, wakati akifungua semina ya kupinga vitendo vya rushwa, Mhandisi Mkuu wa TANESCO Mkoa wa Temeke, David Mhando, amesema kuwa  semina ya kupinga vitendo vya rushwa ni muhimu kwa watumishi wa TANESCO kutokana wanatoa huduma ambayo inamchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa.

Mhandisi Mhando amesema kuwa jukumu la TANESCO ni kuzalisha umeme, kusafirisha pamoja na kusambaza, hivyo kama watumishi wa umma hawatakuwa na uwelewa mpana  kuhusu  rushwa itasababisha utendaji wa kazi kukosa ufanisi na kushamiri vitendo vya rushwa.

“Kuna mazingira mengine mteja au mfanyakazi anaweza kushawishi vitendo vya rushwa, hivyo tumeona tuwaalike TAKUKURU kwa ajili ya kutoa semina yenye lengo kuwaelimisha watumishi wa Mkoa wa Temeka ili waweze kufanya kazi yenye kuleta tija kwa Taifa“ amesema Mhandisi Mhando.

Mhandisi Mhando amesema kuwa lengo ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme iliyokusudiwa bila kupata usumbufu wa aina yoyote kwani ni wajibu wa TANESCO kutoa huduma kwa wateja kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi.

Amesema kuwa kila mtumishi anapaswa kuelewa ni wajibu wake kufanya kazi kwa kuzingatia maadili pamoja na kujua namna ya kuepukana na vitendo vya rushwa katika utekelezaji wa majukumu.

“Kupitia semina hii utendaji, maadili ya watumishi wetu yatakuwa mazuri na wataendelea kutimiza majukumu yao ya kutoa huduma ya umeme kwa Maendeleo ya Taifa letu“ amesema Mhandisi Mhando.

Mhandisi Mhando ametoa wito kwa watumishi wa TANESCO Mkoa wa Temeke kujiepusha na vitendo vya rushwa kwani havikubaliki ndani ya Shirika na kinyume cha sheria za Nchi.

Akitoa mada katika semina hiyo, Mkuu wa Dawati la Elimu kwa Umma TAKUKURU Mkoa wa Temeke Sabina Isuja amesisitiza umuhimu  wa watumishi wa TANESCO kuzingatia maadili katika utendaji wao wa kazi ili kuleta tija na kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Afisa Mawasilinao wa TAKUKURU Mkoa wa Temeke Neema Kilongozi, amesema kuwa rushwa ina madhara makubwa katika utendaji wa TANESCO kutokana inarudisha nyuma maendeleo ya Taifa.

Kilongozi amesema kuwa rushwa inamchango mkubwa kuajiri watumishi wasiokuwa na sifa ambao wanashindwa kutekeleza majukumu yao kikamilifu.

“Rushwa inachangia kutoa huduma kwa upendeleo pamoja na kukatisha tamaa wateja wa nishati na kuwafanya kukosa imani na Shirika la TANESCO lenye jukumu la kuzalisha na kusambaza umeme“ amesema Kilongozi.

Amefafanua kuwa ili kuepukana vitendo vya rushwa mishahara ya watumishi inapaswa kuboreshwa, kutekeleza sera ya rushwa kutoa taarifa kwa usahihi ya vitendo vya rushwa pamoja na kuendelea kujengeana uwezo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *