WIZARA YA MADINI MBIONI KUZINDUA MINING FOR A BRIGHTER TOMORROW

0

Wizara ya Madini iko mbioni kuzindua Programu ya Uchimbaji kwa Kesho Bora (Mining for a Brighter Tomorrow – MBT) yenye lengo la kuwajengea uwezo makundi ya kina mama na vijana wanaojishughulisha na shughuli za Uchimbaji wa Madini pamoja na mnyororo mzima wa Sekta ya Madini nchini.

Hilo limebainishwa na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Madini lililofanyika Mji wa Serikali Mtumba – Jijini Dodoma leo Aprili 8, 2024.

Waziri Mavunde amesema kuwa kupitia Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri, Wizara iko mbioni kuanzisha mpango huo wa Uchimbaji kwa Kesho Bora ili kuongeza tija na manufaa ya uwepo wa rasilimali madini inayopatikana kwa wingi hapa nchini katika kuongeza kipato cha mwananchi mmoja mmoja pamoja na maendeleo ya taifa.

“Ndugu Wajumbe, Muda sio mrefu tutatangaza majina ya wajumbe watakaoongoza ramani ya Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri, ili tufikie malengo tuliyojiwekea, kupitia ramani hii tutaanzisha programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (BMT) itakayowasaidia Wanawake na Vijana kwa kuwapatia maeneo ya uchimbaji na kuwaendeleza ili wanufaike na rasilimali madini na kukuza uchumi wao binafsi pamoja na kuchangia maendeleo ya Sekta ya Madini kwa ujumla” amesema Mavunde.

Amewataka Watumishi wote wa Wizara kuivaa Vision 2030: Madini ni Maisha na Utajiri badala ya kudhani kuwa ni kazi ya Viongozi wa Wizara pekee ili kufikia malengo kwa wakati huku akisema kuwa, milango iko wazi kwa Mtumishi yeyote kushauri namna bora ya kutimiza malengo ya Wizara kwa manufaa ya Sekta ya Madini.

Aidha, Waziri Mavunde amesema kuwa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) linaendelea na mazungumzo na Mwekezaji kwa ajili ya kuja na Mkakati wa kuzalisha Megawati 2000 za Nishati ya Umeme, kiasi kinachokaribia Uwezo wa Mradi wa uzalishaji Umeme wa Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere (JNHPP) na kuonyesha mchango Sekta ya Madini katika kuzalisha nishati ya umeme.

Vilevile, Waziri Mavunde amesema kuwa Wizara itaendelea kuwajengea uwezo wafanyakazi ili kuendelee kutimiza wajibu wao kwa ufanisi mkubwa hatimaye kuwezesha Sekta ya Madini kupiga hatua zaidi katika ukuaji wake pamoja kuongeza Mchango wake katika Pato la Taifa na maendeleo ya uchumi wa nchi kwa ujumla.

Pia, Mhe. Mavunde ameongeza kuwa, Tanzania imejaaliwa kuwa na Madini mengi ikiwemo Madini Muhimu na Mkakati ambayo hivi sasa uhitaji wake ni mkubwa sana duniani kwa ajili ya kuzalisha Nishati Safi kwa mazingira ikiwemo kutengezea betri za magari na kwamba Wizara imejipanga kikamilifu kuhakikisha Tanzania inashiriki Uchumi wa Madini hayo.

Akizungumzia Mkutano huo, Waziri Mavunde amewataka Wajumbe kujadili maeneo muhimu ambavyo ni vipaumbele vya Wizara ikiwa ni pamoja na namna ya Utekelezaji wa Bajeti, Ukusanyaji wa Maduhuli, Uendelezaji wa Miradi ya Maendeleo sambamba na usimamizi mzuri wa Sekta.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Mkutano huo akimwakilisha Katibu Mkuu, amemhakikishia Mheshimiwa Waziri kuwa Wizara na Watumishi wake itatekeleza maelekezo yake kwa maarifa, umakini na weledi kwa kuzingatia uadilifu ili kufikia lengo la Wizara.

Awali, akitoa Taarifa ya Mkutano huo, Mwenyekiti wa TUGHE tawi la Madini, Joseph Ngulumwa amesema kuwa, kwa kuwa Wizara ina fanya kazi kubwa ya kutafuta wawekezaji hivyo, kuna kila sababu ya kuangalia namna bora ya watumishi kuwapeleka kila mwaka katika kampuni zilizopo kufanya kazi kwa muda wa miezi mitatu hadi sita ili kuwajengea uwezo wa tekinojia mpya zinazotumika.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *