BARABARA YA KIDATU-IFAKARA NA DARAJA LA RUAHA

0

KUKAMILIKA MACHI

Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amemtaka

mkandarasi Reynolds Construction Company (RCC), anayejenga

barabara ya Kidatu- Ifakara km 66.9 na daraja la Ruaha lenye

urefu wa mita 133 kuhakikisha ujenzi wa barabara na daraja hilo

unakamilika ifikapo Machi mwaka huu.

Kukamilika kwa daraja hilo linalounganisha wilaya za Kilosa na

Kilombero mkoani Morogoro kutafungua uchumi wa wakazi wa

mikoa ya Morogoro, Njombe, Iringa na Ruvuma kwa kuwa inapita

kwenye eneo lenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya chakula na

biashara.

“Kwa kuwa katika ujenzi huu hakuna changamoto ya fedha hivyo

katika miezi miwili ijayo hakikisheni kazi hii inakamilika na

wananchi wananufaika na uwekezaji huu mkubwa uliofanywa na

Serikali”, amesema Eng. Kasekenya.

Amezungumzia umuhimu wa Wakala wa Barabara nchini

(TANROADS), kushirikiana na mkandarasi kuhakikisha alama

muhimu za usalama barabarani zinawekwa mapema

iwezekanavyo ili kuepusha ajali kwa watumiaji wa barabara hiyo

na kuhakikisha magari yatakayotumia barabara hiyo hayazidishi

uzito.

Kwa upande wake meneja wa TANROADS mkoa wa morogoro

Lazeck Kyamba amemhakikishia Naibu Waziri Kasekenya kuwa

watamsimamia mkandarasi huyo ili kazi zifanywe usiku na

mchana na hivyo kukamilika katika muda mfupi ujao.

Nae mkuu wa wilaya ya Kilombero Dastan Kyobya amesema

kukamilika kwa daraja la ruaha na barabara hiyo kutaleta fursa

nyingi za kiuchumi kwa wakazi wa wilaya hiyo na kuipongeza

TANROADS kwa usimamizi mzuri na shirikishi kwa wananchi.

Katika hatua nyingine naibu waziri kasekenya amekagua

barabara ya mikumi-kilosa hadi dumila ambayo ujenzi wake

unaendelea kwa awamu na kumtaka mkandarasi Umoja JV

anaejenga sehemu ya Rudewa-Kilosa km 22.5 kukamilisha

madaraja matatu ya Mazinyungu, Kobe na Wailonga yaliopo mjini

Kilosa ili kukamilisha mradi huo na kuwawezesha wananchi

kunufaika na mradi huo.

Naibu Waziri Kasekenya yuko mkoani Morogoro kukagua

maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya barabara na madaraja

na kusisitiza umuhimu wa watumiaji wa barabara kuzingatia

sheria ili kuilinda miundombinu hiyo ili idumu kwa muda mrefu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *